
DIAMOND ALIPEWA JET SISI WAKATUPA HELA YA MAFUTA
Mwanamuziki wa Uganda, #EddyKenzo, ameonesha kutoridhishwa na namna wasanii wa ndani walivyotendewa kwenye tamasha la Coffee Marathon lililofanyika hivi karibuni huko Ntungamo, Uganda.
Eddy Kenzo, ambaye aliambatana na mkewe Mbunge Phiona Nyamutoro, alitumbuiza jukwaani lakini alidai kuwa wasanii wa Uganda walipuuzwa huku msanii wa Tanzania, #DiamondPlatnumz, akipewa mapokezi ya kifahari.
“Walimpa Diamond hadhi ya kifalme – jet binafsi, kipaumbele kwenye soundcheck – sisi tukapewa hela ya mafuta tu. Ilikuwa kama sisi si wasanii,” alisema Kenzo kwa masikitiko.
Eddy Kenzo amesema tukio hilo lilikuwa na mpangilio mbovu, huku waandaaji wakimuinua mno Diamond hadi kuwafanya wasanii wa ndani kuonekana hawana thamani.
“Kujifanya kwake staa kulizidi mipaka na kuumiza sekta yetu. Ukarimu ule ungeweza kuelekezwa pia kwa wasanii wa nyumbani,” aliongeza.
Matamshi ya Eddy Kenzo yanaongeza uzito wa mjadala ulioanza mtandaoni kuhusu matumizi ya fedha kubwa kwa msanii mgeni wakati vipaji vya ndani vikipuuzwa. Hii ni changamoto kwa serikali na waandaaji kutafakari jinsi ya kuinua sanaa ya ndani bila kuwatupa wale walio mstari wa mbele kuiendeleza.